Tumsifu Yesu Kristu.
Kesho tunaianza safari ya siku arubaini ya Kwaresma ya mwaka 2025. Mada kuu ya mwaka huu ni KENYA TUNAYOITAMANI. Ziko changamoto nyingi zanazoikumba nchi yetu ya Kenya na kila tunaposali katika kipindi hiki cha Kwaresma, tunahimizwa kuiweka nchi yetu ya Kenya katika sala zetu.
Kwaresma ina majuma sita na huanza na Jumatano ya majivu ambapo wakristu wanapaswa kufunga na kushiriki misa na kupakwa majivu katika siku hii. Tunapopakwa majivu, tunakumbushwa kuwa binadamu ni mavumbi na mavumbini atarudi.
Kwaresma ni safari ya kiroho inayotufundisha kujikana nafsi zetu, kujinyima, na kumkaribia Mwenyezi Mungu zaidi.
Ni wakati wa kutathmini kiroho, kuachana na dhambi na kumruhusu Mungu kufanya kazi maishani mwetu.
Msalaba wa Yesu Kristu unatufundisha kuwa na upendo. Upendo wa hali ya juu, uliomfanya Kristu kujitoa kwa ajili yetu.
Tunapopitia changamoto mbalimbali za maisha, Kwaresma inatufundisha kuwa na uvumilivu na kushikilia imani yetu kwa Mungu, tukijua kuwa mateso tunayopitia ya mwisho na mwishowe tutashinda kama vile Yesu alivyoshinda kifo.
Wakati wa Kwaresma, mimi kama mkristu mkatoliki, ninapaswa kushiriki misa mara nyingi iwezekanavyo, kusali kwa bidii, kusali Rosali, kuenda njia ya msalaba na kusali Novena mbalimbali, kutubu dhambi zetu na kuungama mara kwa mara, kuwa na moyo wa huruma kwa wengine kwa kutoa misaada na kusamehe waliotukosea, kufungua na kujizuia na mambo yanayotufanya tuwe mbali na Mungu na kufanya yale yanayo mpendeza Mungu.
Kwaresma ni kipindi cha kuwa karibu zaidi na Mungu tunapojitahidi kumfuata Kristu kwa kujinyima, kusali na kuwasaidia wengine, tunajiandaa kushiriki kikamilifu furaha ya Pasaka tukisherehekea ushindi wa Yesu juu ya dhambi na kifo.
Tumsifu Yesu Kristu.